KINGAZI BLOG: 09/07/16

HABARI KARIBU YAKO ZAIDI.

Breaking News
Loading...

Wednesday 7 September 2016

Hivi Ndivyo Nilivyofanikiwa Kujiajiri Baada ya Kumaliza Chuo Kikuu

Kwenye kitabu kimoja nilichowahi kusoma, kuna habari ya jeshi lilokwenda vitani. Baada ya wanajeshi wote kuvuka daraja kuwaelekea maadui jemedari mkuu akaamua kuchoma moto lile daraja, magari na kila kitu ambacho kingewawezesha kukimbia ikiwa vita ingewaelemea.

 Kisha akawageukia wanajeshi wake akawaambia, "Chagueni kushinda vita ama kufa kwa sababu kukimbia ama kurudi nyuma haiwezekani tena". Jeshi lile lilishinda vita! Mbinu hii nimepata kuitumia nilipofanya rasmi maamuzi ya kujiajiri pindi nilipomaliza chuo kikuu.

 Nilijua kwenye kujiajiri kuna changamoto nyingi na kuna hatari nikakata tamaa na kutafuta ajira. Nikaamua kuchoma madaraja yote yanayoweza kunifanya nikimbie kujiajiri kwenda kuajiriwa! Kwanza kwa makusudi sikuchukua cheti cha matokeo wala cheti chochote wala barua inayothibitisha nimemaliza chuo kikuu; pili nilijiapiza kutoshughulika na matangazo, habari ama taarifa zozote kuhusu ajira. Nikabaki na option moja tu ya kuhakikisha napambana kufa na kupona kwenye kujiajiri mpaka kieleweke.

 Haikuwa kazi rahisi, lakini sikuwa na namna zaidi ya kutoka ama kufa. Nilikataa kufa na leo ninasonga mbele kwa mafanikio. Ninachokuhakikishia ni kuwa ukiamua kwa moyo mmoja kufanikiwa katika jambo lolote; ni lazima utafanikiwa, no matter what!! Kama stori nzima haijakuvutia, chukua sentensi moja ya mwisho!

 By SmartMind

Aliyefanyiwa upandikizaji wa kwanza wa uso afariki

Madaktari nchini Ufaransa wamefichua kwamba mwanamke aliyefanyiwa upasuaji wa kwanza wa upandikizaji wa sura alifariki mapema mwaka huu.

Hospitali moja imesema kuwa Isabelle Dinoire alifariki baada ya matatizo yanayohusishwa na upasuaji huo .

Alifanyiwa upasuaji huo uliochukua saa 15 mwaka 2005 baada ya kujeruhiwa na mbwa.

Madaktari waliutengeza mdomo wake,pua na taya katika upasuaji huo wa kwanza kuwahi kufanyika.
Hospitali hiyo imesema kuwa kifo chake hakikutangazwa hadi sasa ili kulinda faragha ya familia yake.
Alikuwa na umri wa miaka 49.

Afikishwa Mahakamani kwa Kumtisha Rais Magufuli Kupitia Mtandao wa Watsapp


Mfanyabiasha  Leonard Materu (31) amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, akikabiliwa na mashitaka ya kutuma ujumbe wa kumtishia Rais John Magufuli kupitia mtandao wa WhatsApp.

Materu ambaye ni mkazi wa Moshi Bar Kwadiwani, alifikishwa mahakamani hapo jana na kusomewa mashitaka yake na Wakili wa Serikali, Diana Lukondo mbele ya Hakimu Mkazi Magreth Bankika.

Akisoma mashitaka Wakili Diana alidai, mshitakiwa huyo amefunguliwa kesi hiyo ya kuchapisha taarifa za uongo kwenye mtandao wa WhatsApp chini ya Sheria ya Mtandao ya mwaka 2015.

Ilidaiwa kuwa, Julai 17, mwaka huu jijini Dar es Salaam, Materu aliandika ujumbe wenye lengo la kudanganya umma kupitia WhatsApp ukisomeka; “Magu ajiandae tunaenda kupindua mpaka Ikulu.”

Inadaiwa kuwa maneno hayo yalikuwa na lengo la kumtishia Rais John Magufuli. Baada ya kusomewa mashitaka, mshitakiwa alikana kutenda kosa hilo, na upande wa Jamhuri ulidai kuwa upelelezi wa kesi haujakamilika na kuomba tarehe nyingine ya kutajwa.

Mshitakiwa aliachiwa kwa dhamana baada ya kutimiza masharti ya dhamana ya kuwa na wadhamini wawili ambao kila mmoja alisaini hati ya Sh milioni tano. Kesi itatajwa tena Septemba 20, mwaka huu.

Mtindo wa kutambulisha wageni bungeni ‘kupigwa stop’


BUNGE linakusudia kuachana na mtindo wa kutambulisha wageni baada ya kipindi cha maswali na majibu kuanzia mkutano ujao wa Bunge isipokuwa kwa wageni wa kimataifa, lengo likiwa kuokoa muda wa shughuli za chombo hicho cha kutunga sheria nchini.

Hayo yalisemwa bungeni mjini hapa na Spika wa Bunge, Job Ndugai aliyeliongoza Bunge hilo kwa mara ya kwanza baada ya miezi kadhaa ya kuwa nje ya nchi alikokwenda kwa matibabu.

Alisema hayo baada ya kuongoza kipindi cha maswali na majibu na kusisitiza hayo yametokana na mapendekezo ya Kamati ya Uongozi ya Bunge.

“Kuanzia Bunge lijalo hatutambulisha wageni, labda wale wa kimataifa kwa sababu Watanzania tuko nao kila siku, si wageni katika nchi hii,” alisema Ndugai.

Tangazo hilo liliibua vicheko kwa wabunge, wanahabari na wageni waliokuwamo bungeni huku wengi wakionekana kukubaliana ikielezwa itasaidia kuokoa muda wa shughuli za Bunge.

Hata hivyo, alisema kama kuna wabunge wenye mawazo tofauti, bado wana fursa ya kuwasilisha ili yafanyiwe kazi kuona uzito wa hoja zitakazojengwa.

Kwa muda mrefu sasa, wageni mbalimbali wa wabunge wamekuwa wakifurika wakati wa vikao vya Bunge na wamekuwa wakitambulishwa bungeni, hali iliyotajwa kuchukua muda mwingi wa shughuli za Bunge.

MAGAZETI YA LEO JUMATANO,SEPT 07,2016 KWENYE HEADLINES ZA KITAIFA KIMATAIFA MICHEZO NA BURUDANI.

  Karibu , Tunakuletea baadhi ya habari zilizopewa uzito kwenye magazeti ya leo jumatano














WATAHINIWA 795,761 KUFANYA MTIHANI WA KUMALIZA ELIMU YA MSINGI LEO NA KESHO TANZANIA


WATAHINIWA 795,761 wanatarajia kufanya Mtihani wa Kumaliza Elimu ya Msingi (PSLE) unaofanyika leo na kesho nchini kote. 

Akizungumza Dar es Salaam jana, Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA), Dk Charles Msonde alisema wanafunzi 372,883 ambao ni sawa na asilimia 46.86 ni wavulana na wasichana ni 422,878 ambao ni asilimia 53.14. 

Mwaka 2015 watahiniwa waliosajiliwa kufanya mtihani walikuwa 775,729 huku 763,602 ndio waliofanya mtihani huo na wanafunzi 518,034 walifaulu. 

Dk Msonde alisema watahiniwa 765,097 watafanya mtihani kwa lugha ya Kiswahili na watahiniwa 30,664 watafanya mtihani kwa lugha ya Kiingereza ambayo wamekuwa wakiitumia katika kujifunzia. Masomo yatakayotahiniwa ni Kiswahili, Kiingereza, Sayansi, Hisabati na Maarifa.

Alisema watahiniwa wasioona waliosajiliwa kufanya mtihani ni 95 wakiwemo wavulana 57 na wasichana 38 wakati wale wenye uoni hafifu ambao huhitaji maandishi makubwa ni 810 ambao kati yao wavulana ni 402 na wasichana ni 408. 

“Maandalizi yote kwa ajili ya mtihani huo yamekamilika kiwa ni pamoja na kusambazwa kwa karatasi za mitihani, fomu maalum za kujibia mtihani na nyaraka zote muhimu katika halmashauri na manispaa zote nchini,” alisema Dk Msonde. 

Aidha, Dk Msonde alitoa mwito kwa kamati za mitihani za mikoa na halmashauri kuhakikisha taratibu za mitihani ya Taifa zinazingatiwa ikiwa ni pamoja na kuhakikisha mazingira ya vituo vya mitihani yanakuwa salama, tulivu na kuzuia mianya ya udanganyifu. 

“Wasimamizi wanatakiwa kusimamia kwa umakini na uadilifu wa hali ya juu. Nawaaasa kujiepusha na vitendo vya udanganyifu kwani Baraza litachukua hatua kali kwa yeyote yule atakayebainika kukiuka taratibu za uendeshaji wa mitihani ya Taifa,” alieleza.

Na Anastazia Anyimike
 

Gallery

Popular Posts

About Us