KINGAZI BLOG: 08/30/16

HABARI KARIBU YAKO ZAIDI.

Breaking News
Loading...

Tuesday 30 August 2016

Lipumba: Mimi bado ni Mwenyekiti wa CUF, sitambui kikao cha Zanzibar

Image result for lipumba leo
Jamani, ngoma sasa inogile. Prof. leo kakomaa hataki kabisa kuambiwa amesimamishwa uanachama.

Hii safi sana maana maalim anaendesha chama kama mali yake.

Akihojiwa na mtangazaji Spencer Lamerk wa ITV usiku huu, Prof. Ibrahim Haruna Lipumba amesema kuwa yeye bado ni Mwenyekiti halali wa CUF.

Prof. Lipumba amesema kuwa kufuatia kutengua barua yake ya kujiuzulu Uenyekiti, aliandika barua kwa Katibu Mkuu wake kutaka kurejea kazini kama Mwenyekiti. Katibu Mkuu alimjibu kuwa anatafuta ushauri wa kisheria.

Kuhusu kikao cha Baraza Kuu la CUF kilichomsimamisha uanachama, Profesa Lipumba amesema kuwa kikao hicho hakikuwa halali kwakuwa hakukuwa na akidi ya Wajumbe wa kutoka Tanzania Bara. Amesema kuwa Katibu Mkuu hamshirikishi Naibu Katibu Mkuu Bara na kuonekana akiendesha chama kiimla.

Prof. Lipumba amesema kuwa Katibu Mkuu asipotaja tarehe ya yeye kurejea kazini kama Mwenyekiti, atasubiri barua ya Msajili wa Vyama ili aanze kazi tena kama Mwenyekiti wa taifa wa CUF.

Maghembe apiga marufuku usafirishaji mbao usiku

Waziri wa Maliasili na Utalii Prof. Jumanne Maghembe amewataka wafanyabiashara waliopewa vibali vya kuvuna na kuuza bidhaa za misitu hususani mbao, kusafirisha mizigo yao nyakati za mchana ili kuepuka udanganyifu unaofanywa na baadhi ya wafanyabiasha.
Profesa Maghembe ametoa agizo hilo leo Jijini Dar es Salaam, wakati wa mkutano baina yake na wadau wa masuala ya misitu, mkutano ambao pamoja na mambo mengine ulikuwa unajadili uvunaji holela wa rasilimali za misitu.
Kwa mujibu wa Waziri Maghembe, tabia ya kusafirisha mbao nyakati za usiku imekuwa ni moja ya njia inayotumiwa katika ukwepaji wa ushuru pamoja na uvushaji wa mbao zilizovunwa kwenye aina ya miti ambayo haistahili kuvunwa.

SERIKALI KUTOA AJIRA MPYA 71, 496 HIVI KARIBUNI

SERIKALI imeanza kuwashughulikia watumishi walionufaika na fedha za watumishi hewa ambapo hadi sasa watumishi 839 wapo katika hatua mbalimbali wakiwemo waliofikishwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na wengine wanaendelea kuhojiwa polisi kwa ajili ya kufikishwa mahakamani.
Sambamba na hilo, serikali inatarajia kutoa ajira mpya 71,496 kwa mwaka huu wa fedha baada ya kukamilisha uondoaji wa wafanyakazi hewa. 
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora), Angella Kairuki aliyasema hayo wakati akizungumzia utekelezaji wa mipango na mikakati ya wizara yake katika kipindi cha ‘Tunatekeleza’ kinachorushwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC1). Kairuki alisema,
“Kwa sasa tayari wapo watumishi wameshahojiwa na kuchukuliwa maelezo yao polisi na upelelezi utakapokamilika watachukuliwa hatua mbalimbali za kisheria, ikiwemo kufikishwa mahakamani… Tunakamilisha ushahidi na tutawatangazia tutakapokamilisha,”alisema.
Alisema waligundua kwamba kuna maofisa utumishi na wahasibu ambao siyo waaminifu, badala yake walikuwa wakielekeza fedha kwa ndugu zao na miradi yao na wengine walishastaafu lakini bado majina yao yalikuwa yakiendelea kupokea mishahara wakati walitakiwa kuondolewa kwenye mfumo.Alisema kwa kipindi cha Machi mosi hadi Agosti 20 mwaka huu, watumishi hewa waliogundulika ni zaidi ya 16,127 na kuisababishia serikali hasara ya mabilioni ya fedha. Kwa kipindi cha Agosti pekee watumishi hao hewa wangelipwa mishahara wangeisababishia serikali hasara ya zaidi ya Sh bilioni 16.
“Uhakiki huu ni endelevu na tumegundua changamoto kubwa katika usimamizi wa mishahara ni uadilifu kwa watu waliokasimiwa madaraka. Maofisa Utumishi, Maofisa Utawala na Wahasibu wamepewa madaraka lakini wengi wao siyo waaminifu, hivyo kwa sasa tumeweka uwajibikaji kwa waajiri,” alisema.Aidha alisema wanaufanyia mfumo wao maboresho zaidi ili uweze kuchakata taarifa nyingi zaidi ambapo pia sekta ya mishahara imeshushwa katika ngazi za chini zaidi hasa katika sekta za elimu na afya ambazo zimekutwa na watumishi hewa wengi zaidi ili waweze kuwa na taarifa za mtumishi mmoja mmoja.Alisema upo muongozo ambao fedha za serikali zinaporejeshwa zinapitia hazina na kusisitiza kwamba wataendelea kuhakikisha wanasimamia fedha zote ambazo zilichukuliwa serikalini kinyume na utaratibu na isivyo halali zinarudishwa kwa mfumo sahihi.
Pia alisema wameongeza kasi ili kuhakikisha kunakuwa na nidhamu ya kazi na uwajibikaji kwa watumishi wa umma, hivyo wanaanda mkataba wa utendaji kazi kwa watumishi wa umma na ikiwezekana utaanza kutumika mwaka ujao wa fedha.
Alisema serikali imefanya maboresho makubwa katika mishahara na motisha kwa ajili ya maslahi ya watumishi wa umma, sambamba na kuhimiza taasisi mbalimbali kuweka vitendea kazi ili kuwawezesha wafanyakazi kutekeleza majukumu yao ipasavyo.
Akizungumzia ajira hizo mpya Kairuki aliwatoa hofu watanzania waliokuwa wanatarajia ajira serikalini na kusisitiza kwamba walichokuwa wanasubiri ni takwimu halisi kwa taasisi ili kujua ni watumishi wangapi wameondolewa.
“Baada ya kukamilisha mchakato huo, hatua nyingine zitaendelea… Hii ni neema kwa waliomaliza vyuo, cha msingi wavute subira maana tutatoa ajira 71,496 kwa mwaka huu wa fedha na hatukuzifuta ajira. 
"Nawashauri vijana wasijiingize kwenye makundi yasiyofaa wasubiri ajira zinakuja,”alisema. 
Katika hatua nyingine, Kairuki alisema, wamepokea malalamiko zaidi ya 200 kutokana na ukiukwaji wa sheria ya maadili ya viongozi wa Utumishi wa Umma ambayo inamnyima mtumishi kutotumia madaraka yake vibaya.
“Katika malalamiko hayo 142 yanahusu sheria ya maadili. Sekretarieti ya Maadili imefanya uchunguzi wa awali na malalamiko 12 yataanza kufikishwa Baraza la Maadili na hatua mbalimbali zinaweza kuchukuliwa ikiwemo kushushwa vyeo au kuachishwa kazi,”alisema.
Pia aliwaagiza maofisa utumishi kuwahudumia watumishi na kuwapa haki zao ikiwemo kuwapandisha madaraja kwa wakati pale wanapostahili. Aidha Kairuki alikemea tabia ya baadhi ya watu kughushi taarifa za utumishi wa umma na kusisitiza kwamba jambo hilo ni kosa kubwa kwa yeyote anayefanya hivyo.
“Mtu yeyote ambaye anatoa nyaraka za serikali na siyo mlengwa au anayetoa nyaraka ambayo imewekewa zuio kwa mujibu wa sheria ni kosa la jinai na hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake. Tunawasisitiza watumishi wa umma kuhakikisha wanazingatia sheria hizo na mwongozo wa utoaji nyaraka na kumbukumbu za taarifa za serikali,”alisema.

Hebu muone Nick Minaj katika vazi hili

HILI NDIO VAZI LA NICKI MINAJ ALILOVAA KWENYE TUZO ZA VMAS


 

UVCCM WASALIMU AMRI ... WAAHIRISHA MAANDAMANO YAO

Agosti 22, 2016 Umoja wa Vijana wa CCM tuliutangazia umma na dunia kwamba ifikapo Agosti 31 mwaka huu tutaitisha maandamano ya amani nchi nzima yenye lengo la kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais Dk John Pombe Magufuli kwa utendaji wenye tija, ufanisi na uliorudisha imani na matumaini kwa wananchi. Msimamo na dhamira ya kufanya maandamano hayo ya amani yenye maudhui na kusudio hilo, bado uko pale pale ingawaje si kwa tarehe tuliopanga na kutangaza awali yaani Agosti 31 mwaka huu. Jumuiya yetu kama mjuavyo ni ya Vijana wa CCM, (UVCCM) inapata malezi kwa karibu mno na Jumuiya ya Wazazi ya CCM. Wiki ya jana Mwenyekiti wa Wazazi Taifa Nd. Abdallah Bulembo alikutana na waandishi wa habari akitutaka UVCCM tuahirishe maandamano ya Agosti 31 mwaka huu hadi wakati mwingine. Kwa mujibu wa Katiba ya Chama Cha Mapinduzi, Jumuiya ya Wazazi ndiyo Msimamizi wa Malezi, Maadili na Adabu kwa Vijana wote nchini, sisi UVCCM tunaamini kuwa sikio halishindani na kichwa, mtoto ni mtoto kwa Wazazi wake hakui, hana jeuri wala ubishi. Mtoto au watoto wanaokaidi amri, ushauri au maelekezo ya Wazazi wao huitwa watukutu, wenye viburi, manunda na wasioambilika. UVCCM si watukutu, hatukufunzwa tuwe wabishi, wakaidi na wenye viburi. Tumezingatia kutii maelekezo, makatazo na maonyo , tumeambiwa tuahirishe maandamano yetu nasi tumekubali na kuheshimu mambo tuliyoaswa. Sambamba na hilo tumepata majibu ya barua yetu tuliyomwandikia Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP Ernes Mangu) inayotutaka tuache kufanya maandamano yetu kwa sababu Polisi wamezuia mikutano ya hadhara ya Vyama vya Siasa na maandamano nchi nzima. Jambo jingine ambalo limetufanya pia tuahirishe maandamano yetu ya Amani ni taarifa ya kintelejinsia iliowasilishwa na Kamati yetu ya Usalama na Maadili ya UVCCM mbele ya kikao cha Sekreteriet yetu, nayo ilipendekeza suala hilo liahirishwe kwa wakati huu hadi muda mwingine. Pia jambo jingine ambalo limefanya maandamano hayo tuyabatilishe ni kulipisha Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ ) ambalo litakuwa katika shughuli za maadhimisho miaka 52 tokea kuanzishwa kwake.  Wanajeshi wetu watakuwa katika kazi mbalimbali za kijeshi kwenye kambi zao na mitaani kufanya usafi wa mazingira, hivyo isingependeza na wala si heshima wakati sisi tukiandamana, wao wakifanya kazi muhimu kila mmoja wetu zinazomgusa badala yake ni vyema kuwaunga mkono jambo wanalolifanya la usafi wa mazingira.  UVCCM tumekubali, hatutaki kuingia katika uvunjaji wa sheria hasa baaada ya kutakiwa kuahirisha na mamlaka za Kisheria hadi wakati mwingine muafaka na si wakati huu. Tunaelewa kwamba uamuzi wetu wa awali wa kutaka kuandamana kwa amani hata kama tungenyimwa kibali ungetugharimu, ungetusababishia madhara na pengine hasara, kwa wakati huu na kuona jambo lenyewe ni la kuipa Ari serikali katika kuhimiza Uwajibikaji, Utendaji na Usimamizi bora wa Uendeshaji wa masuala ya kiutawala. Tulishusha maagizo kwa Makatibu wetu wote wa Mikoa yote 32 na Wilaya 171 ya Kichama tukiwataka waandike barua katika Ofisi za Ma RPC na OCD, washirikiane ili kuratibu maandamano na kuyafanikisha kama tulivyokusudia. Watendaji wetu wa ngazi husika wamefuata maelekezo, wametii taratibu zetu za kiutendaji na leo tumewajulisha tena wasitishe maandamano hadi tutakapowapa tena maelekezo mengine. Tunawahimiza na kuwataka ni vyema kutii mamlaka za Kikanuni na Kisheria. UVCCM kwa wakati huu tumeamua kuachana na maandamano badala yake tunajikita katika matayarisho ya kuwapeleka Vijana wetu wakashiriki katika Mafunzo ya Siasa, Utawala, Uongozi, Ufundi na Ujasiriamali yatakayoanza kufanyika katika Chuo chetu kilichopo huko Ihemi Mkoani Iringa ambapo kitakuwa kielelezo na alama nzuri ya kumuunga mkono Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli kwa vitendo. Tumewataka Makatibu wetu wa Mikoa na Wilaya kuendelea na zoezi la Uratibu na Uhakiki kwa Vijana ambao watateuliwa kushiriki Mafunzo hayo huko Ihemi. UVCCM tunarejea kusema tena kwamba dhamira ya maandamano yetu ya kusifu Utendaji wa Serikali ya awamu ya tano iko pale pale ila tutapanga tarehe nyingine katika wakati ujao badala ya kufanyika Agosti 31 mwaka huu kama tulivyotangaza hapo awali. UVCCM tunawataka Vijana wote kuendelea kuheshimu Tunu ya Amani Umoja na Mshikamo wetu kwa Taifa. KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI Shaka Hamdu Shaka (MNEC) KAIMU KATIBU MKUU.

Waziri Mkuu Akaribisha Wawekezaji Kutoka Japan.

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewakaribisha wawekezaji kutoka Japan na kusema kwamba kufanyika kwa Mkutano wa Sita wa Kimataifa wa Tokyo kuhusu Maendeleo ya Bara la Afrika (TICAD VI) jijini Nairobi kumetoa fursa kwa Tanzania na nchi nyingine kukutana na wafanyabiashara wakubwa wenye nia ya kuwekeza barani humo.
Ametoa kauli hiyo Jumapili, Agosti 28, 2016 alipokutana faragha kwa nyakati tofauti na viongozi wa makampuni makubwa ya Japan ambao walikuwa wakihudhuria mkutano huo uliofanyika katika kituo cha Mikutano ya Kimataifa cha Jomo Kenyatta (JICC) jijini Nairobi, Kenya.
Mkutano wa sita wa TICAD ambao umemalizika jana, ulilenga kuiwezesha Afrika katika sekta ya uchumi na uwekezaji. Ili kufikia lengo hilo, mkutano huo umewashirikisha wadau wa sekta binafsi zikiwemo kampuni binafsi zaidi ya 300 kutoka Japan.
Katika mazungumzo yake na Waziri Mkuu, Rais wa kampuni ya Sumitomo, Bw. Kuniharu Nakahura, alisema kampuni hiyo imeanza utekelezaji wa mradi wa Kinyerezi II wa kuzalisha umeme wa MW240 kutoka gesi asilia (Gas Fired Combined Cycle Gas Power Plant). Mradi huo ulioanza kutekelezwa Machi 2016, unatarajiwa kukamilika ndani ya miaka mitatu.
Bw. Nakahura ambaye pia ni Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo, alisema kampuni yao inajishughulisha zaidi na utengenezaji wa bidhaa za vyuma, kemikali, ujenzi wa miundominu, na usafirishaji.
Naye Makamu wa Rais wa kampuni ya Toyota Tshuso, Bw. Yasuhiko Yokoi alikutana na Waziri Mkuu na kumweleza jinsi kampuni hiyo kubwa duniani inavyoweza kushiriki na kuchangia maendeleo nchini Tanzania.
Alisema kampuni yao inajishugulisha zaidi na masuala ya miundombinu ikiwemo kuzalisha mitambo ya umeme na mitambo ya bandari. Pia inazalisha bidhaa za kilimo (matrekta, mashine za viwanda vya mbolea na nguo, ujenzi wa maghala ya nafaka), mitambo ya nguvu za umeme wa joto-ardhi na uzalishaji wa magari ya aina mbalimbali.
“Kwa mfano hapa Kenya, tumeweza kutengeneza mitambo midogo ya kisasa ambayo inazalisha mbolea tofauti kulingana na hali halisi ya udongo wa mahali husika. Huwezi kuzalisha mbolea ya aina moja na kuamua kuisambaza kwa nchini nzima. Tunapima udongo wa sehemu moja na kuzalisha mbolea inayofaa kwa udongo ule,” alisema.
Naye Rais wa kampuni ya Marubeni, Bw. Fumiya Kokubu alimweleza Waziri Mkuu kwamba maeneo ambayo wangependa kuwekeza ni kwenye viwanda vya nguo, mbolea, saruji, uzalishaji wa sukari, umeme wa gesi na hasa miradi ya LNG.
Kwa upande wake, Waziri Mkuu aliwahakikishia wawekezaji hao kuwa Serikali iko tayari kushirikiana nao na akawashauri watume timu za maafisa wao ili wakutanishwe na wadau wa sekta husika.
Alisisitiza kuwa Tanzania hivi sasa imedhamiria kuwa nchi ya uchumi wa viwanda na kwa sababu hiyo inahitaji kuwa na nishati ya kutosha ili iweze kumudu kuendeleza sekta hiyo. “Serikali ya awamu ya tano imeamua kujenga uchumi wa viwanda, tunahitaji kujenga viwanda vya kutosha ili tuweze kusindika mazao ya wakulima ambao wanafikia asilimia 80 ya Watanzania wote. Tunahitaji masoko ya uhakika kwajili ya mazao wanayozalisha,” alisema.
Akiwa kwenye mkutano huo, Waziri Mkuu pia alikutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Umoja wa Mataifa anayeshughulikia masuala ya wakimbizi, Bw. Filippo Grandi; Meya wa Jiji la Yokohama, Bibi Fumiko Hayashi; na Makamu wa Rais wa Kwanza wa Sudan, Jenerali Bakri Hassan Saleh.
Wakati huohuo, Waziri Mkuu alitembelea Maonesho ya Biashara ya Afrika na Japan (Africa-Japan Expo 2016) ambapo Mamlaka ya Kuendeleza Biashara Tanzania (TANTRADE) na wadau wengine kama Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA), Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Mamlaka ya Ukanda Maalumu wa Uwekezaji (EPZA) walishiriki.
Akiwa huko alitembelea pia mabanda ya Uganda, Rwanda, Sénégal, Kenya, Japan na UN Habitat. Pia alitembelea banda la wajasiriamali wa nguo kutoka Tanzania ambao walishiriki maonyesho hayo yaliyofanyika kwenye viwanja vya Kituo cha Mikutano ya Kimataifa cha Jomo Kenyatta (JICC) jijini Nairobi, Kenya.
Waziri Mkuu alirejea jijini Dar es Salaam jana usiku.
(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMATATU, AGOSTI 29, 2016.

Lipumba Aendelea Kung'ang'ania Uenyekiti Wake CUF


Katika hali isiyokuwa ya kawaida Prof Lipumba ameendelea Kung’ang’ania kiti cha uenyekiti wa chama chake cha CUF na kusema kikao kilichokaa jana visiwani Zanzibar na kufanya maamuzi ya kuwasimamisha uanachama, hakikuwa halali na kilikuwa nje ya katiba ya CUF, sababu mojawapo ikiwa ni kuwekwa kando kwa Naibu Katibu Mkuu Bara, Magdalena Sakaya.
“Kikao hicho hakikuwa halali, haiwezekani Baraza Kuu linakaa halafu Naibu Katibu Mkuu Bara hajui, wala hakujulishwa, na bado kuna wajumbe wengine hawakuhusishwa” Alisema Prof Lipumba
Lipumba aliongeza kuwa ni kweli alijiuzulu uenyekiti, lakini baadaye aliamua kuandika barua kwa Katibu Mkuu ya kutengua uamuzi wake wa kujiuzulu na sasa yeye ndiye Mwenyekiti halali wa chama hicho.
“Nilimuandikia barua ya kurudi kwenye nafasi yangu, akasema anasubiri ushauri wa kisheria, lakini hadi sasa hakuna kitu, hiyo inamaanisha kuwa sasa mimi naendelea na nafasi yangu, na niko ngangari kama mwenyekiti” Alisema Prof Lipumba.
Aidha aliongeza kuwa alitaka kujieleza katika mkutano mkuu mbele ya wanachama, lakini mkutano ule ukavurugwa.
Kuhusu kuwepo kwa tofauti kati yake na Katibu Mkuu wa chama hicho Maalim Seif Sharif Hamad, Prof Lipumba amesema kuwa huenda kuna tofauti kwa kuwa mara nyingi huwa hamuAelewi jinsi anavyokiendesha chama bila kifuata misingi ya kidemokrasia.
“Katibu Mkuu anamdharau na hampi heshima yake Naibu Katibu Mkuu Bara, mara nyingi huamua mambo yake bila kushirikisha viongozi wengine, halafu sasa anataka kufukuza wanachama, huwezi kuwa na chama halafu ufukuze wanachama, wanachama wanatafutwa duniani kote, halafu wewe unawafukuza, hizo ni dalili za uongozi wa kiimla, kuongoza chama unapaswa kujali demokrasia na siyo kuwa dikteta ndani ya chama” Amesema
Kuhusu Julius Mtatiro kuwa mwenyekiti mpya wa Kamati ya Uongozi, Lipumba amesema kuwa hatambui maamuzi hayo, na wala hamtambui Mtatiro kama kiongozi wa chama hicho bali mjumbe wa Mkutano Mkuu, nafasi ambayo yeye ndiye aliyempa.
“Mtatiro hawezi kuwa mwenyekiti, mimi ndiye mwenyekiti wa chama, Mtatiro alishindwa hata kuongoza mkutano mkuu, ukavurugika, hawezi, simtambui”

Taarifa Kwa Umma Kuaribika Kwa Mashine ya MRI Hospitali ya Taifa Muhimbili

Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) inapenda kuujulisha umma kwamba mashine ya MRI itasimama kwa muda kufanya kazi baada ya kuharibiika. Mashine hii iliharibiika tarehe 24/08/2016 baada ya kutokea hitilafu ya umeme.

Baada ya kuharibiika, tarehe hiyo (24/08/2016) mafundi wa Philips kwa kushirikiana na mafundi wetu walianza kutafuta athari baada ya kutokea kwa hitilafu ya umeme.

Tarehe 26/08/2016, mafundi walibadilisha betri zote 31 na kufunga mpya ili kuongeza ufanisi katika mashine hii kwa kuwa betri za awali zilikuwa zimefungwa muda mrefu. Tarehe 28/08/2016 mafundi walibaini kwamba kifaa cha Gradient Module kilikuwa kimeharibiika na tayari hospitali kwa kushirikiana na Philips wameagiza kifaa hicho kutoka Uholanzi.

Hospitali ya Taifa Muhimbili inawaomba radhi wananchi kwa usumbufu wowote uliojitokeza.

Imetolewa na;

                                                                                         John Stephen, Ofisa Uhusiano,

                                                                                        

                                                                                         Hospitali ya Taifa Muhimbili

Mchezaji Mpira Avunjiwa Mkataba Baada ya Kugundulika Ana Virusi vya Ukimwi

Zikiwa zimepita siku nne tu tangu asajiliwe na klabu ya Al Ittihad inayoshiki ligi kuu ya Misri, Samuel Nlend, 21, mkataba wake umevunjwa baada ya klabu yake mpya kugundua mchezaji huyo anamaambukizi ya Virusi Vya Ukimwi (VVU).

Jarid linalojulikana kwa jina la KingFut.com limeripoti kuwa, afisa habari wa klabu hiyo amethibitisha taarifa hiyo ya kusikitisha kwa vyombo vya habari.

Mshambuliaji huyo ameitumikia Cameroon katika michezo mitano, alifunga goli January kwenye michuano ya mataifa ya Afrika kabla ya kujiunga na Al Ittihad majira ya kiangazi.

Samuel Nlend alisaini mkataba wa miaka mitatu kuitumikia Al Ittihad tangu tarehe 24 August. Licha ya hayo yote kutokea bado amepata support ya kutosha kutoka kwa klabu yake mpya ya Misri.

Waliochuma watumishi hewa matatani

SERIKALI imeanza kuwashughulikia watumishi walionufaika na fedha za watumishi hewa ambapo hadi sasa watumishi 839 wapo katika hatua mbalimbali wakiwemo waliofikishwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na wengine wanaendelea kuhojiwa polisi kwa ajili ya kufikishwa mahakamani.

Sambamba na hilo, serikali inatarajia kutoa ajira mpya 71,496 kwa mwaka huu wa fedha baada ya kukamilisha uondoaji wa wafanyakazi hewa. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora), Angella Kairuki aliyasema hayo wakati akizungumzia utekelezaji wa mipango na mikakati ya wizara yake katika kipindi cha ‘Tunatekeleza’ kinachorushwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC1). Kairuki alisema,

“Kwa sasa tayari wapo watumishi wameshahojiwa na kuchukuliwa maelezo yao polisi na upelelezi utakapokamilika watachukuliwa hatua mbalimbali za kisheria, ikiwemo kufikishwa mahakamani… Tunakamilisha ushahidi na tutawatangazia tutakapokamilisha,” alisema.

Alisema waligundua kwamba kuna maofisa utumishi na wahasibu ambao siyo waaminifu, badala yake walikuwa wakielekeza fedha kwa ndugu zao na miradi yao na wengine walishastaafu lakini bado majina yao yalikuwa yakiendelea kupokea mishahara wakati walitakiwa kuondolewa kwenye mfumo.

Alisema kwa kipindi cha Machi mosi hadi Agosti 20 mwaka huu, watumishi hewa waliogundulika ni zaidi ya 16,127 na kuisababishia serikali hasara ya mabilioni ya fedha. Kwa kipindi cha Agosti pekee watumishi hao hewa wangelipwa mishahara wangeisababishia serikali hasara ya zaidi ya Sh bilioni 16.

“Uhakiki huu ni endelevu na tumegundua changamoto kubwa katika usimamizi wa mishahara ni uadilifu kwa watu waliokasimiwa madaraka. Maofisa Utumishi, Maofisa Utawala na Wahasibu wamepewa madaraka lakini wengi wao siyo waaminifu, hivyo kwa sasa tumeweka uwajibikaji kwa waajiri,” alisema.

Aidha alisema wanaufanyia mfumo wao maboresho zaidi ili uweze kuchakata taarifa nyingi zaidi ambapo pia sekta ya mishahara imeshushwa katika ngazi za chini zaidi hasa katika sekta za elimu na afya ambazo zimekutwa na watumishi hewa wengi zaidi ili waweze kuwa na taarifa za mtumishi mmoja mmoja.

Alisema upo muongozo ambao fedha za serikali zinaporejeshwa zinapitia hazina na kusisitiza kwamba wataendelea kuhakikisha wanasimamia fedha zote ambazo zilichukuliwa serikalini kinyume na utaratibu na isivyo halali zinarudishwa kwa mfumo sahihi.

Pia alisema wameongeza kasi ili kuhakikisha kunakuwa na nidhamu ya kazi na uwajibikaji kwa watumishi wa umma, hivyo wanaanda mkataba wa utendaji kazi kwa watumishi wa umma na ikiwezekana utaanza kutumika mwaka ujao wa fedha.

Alisema serikali imefanya maboresho makubwa katika mishahara na motisha kwa ajili ya maslahi ya watumishi wa umma, sambamba na kuhimiza taasisi mbalimbali kuweka vitendea kazi ili kuwawezesha wafanyakazi kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Akizungumzia ajira hizo mpya Kairuki aliwatoa hofu watanzania waliokuwa wanatarajia ajira serikalini na kusisitiza kwamba walichokuwa wanasubiri ni takwimu halisi kwa taasisi ili kujua ni watumishi wangapi wameondolewa.

“Baada ya kukamilisha mchakato huo, hatua nyingine zitaendelea… Hii ni neema kwa waliomaliza vyuo, cha msingi wavute subira maana tutatoa ajira 71,496 kwa mwaka huu wa fedha na hatukuzifuta ajira. Nawashauri vijana wasijiingize kwenye makundi yasiyofaa wasubiri ajira zinakuja,” alisema. Katika hatua nyingine, Kairuki alisema, wamepokea malalamiko zaidi ya 200 kutokana na ukiukwaji wa sheria ya maadili ya viongozi wa Utumishi wa Umma ambayo inamnyima mtumishi kutotumia madaraka yake vibaya.

“Katika malalamiko hayo 142 yanahusu sheria ya maadili. Sekretarieti ya Maadili imefanya uchunguzi wa awali na malalamiko 12 yataanza kufikishwa Baraza la Maadili na hatua mbalimbali zinaweza kuchukuliwa ikiwemo kushushwa vyeo au kuachishwa kazi,” alisema.

Pia aliwaagiza maofisa utumishi kuwahudumia watumishi na kuwapa haki zao ikiwemo kuwapandisha madaraja kwa wakati pale wanapostahili. Aidha Kairuki alikemea tabia ya baadhi ya watu kughushi taarifa za utumishi wa umma na kusisitiza kwamba jambo hilo ni kosa kubwa kwa yeyote anayefanya hivyo.

“Mtu yeyote ambaye anatoa nyaraka za serikali na siyo mlengwa au anayetoa nyaraka ambayo imewekewa zuio kwa mujibu wa sheria ni kosa la jinai na hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake. Tunawasisitiza watumishi wa umma kuhakikisha wanazingatia sheria hizo na mwongozo wa utoaji nyaraka na kumbukumbu za taarifa za serikali,” alisema.

MAGAZETI YA LEO JUMANNE YA TAR 30 AUGUST 2016 KWENYE HEADLINES ZA KITAIFA UDAKU, NA MICHEZO. 





 

Gallery

Popular Posts

About Us