KINGAZI BLOG: 04/02/17

HABARI KARIBU YAKO ZAIDI.

Breaking News
Loading...

Sunday 2 April 2017

Chama cha Wamiliki wa Mabasi(TABOA) kimetangaza Mgomo kuanzia wiki ijayo.

 Image result for KITUO CHA  MABASI


Chama cha Wamiliki wa Mabasi(TABOA) kwa kushirikiana na Wamiliki wa Malori na Chama cha Wasafirishaji Mkoa wa Dar es Salaam kimetangaza mgomo wa usafirishaji abiria na mizigo nchi nzima kuanzia siku ya jumatatu ili kushinikiza serikali kutopitisha sheria ya usafirishaji inayotarajiwa kusomwa mara ya tatu na kupitishwa siku ya Jumanne wiki ijayo.

Akitoa maazimio hayo yaliyofikiwa katika mkutao mkuu maalumu wa chama cha wamiliki wa Mabasi, Malori, Daladala na Baji, katibu mkuu wa TABOA Bwana. Eneo Mrutu amesema sheria inaloyolenga kupitishwa haikuwashirikisha wadau na haitenganishi makosa ya dereva na mmiliki, hali inayosababisha kosa lililofanywa na dereva linasababisha mmiliki kufungwa jela.

Aidha amewaomba wabunge bila kujali itikadi za vyama vyao kutopisha sheria hiyo mpaka ifanyiwe marekebisho kwa kuwa inalenga kuharibu sekta ya usafirishaji nchini.

Chanzo: ITV

Tundu Lissu: "Nilinusurika kupigwa na Wasira"

Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lisu alinusurika kushambuliwa na mbunge wa zamani wa Bunda, Steven Wasira katika moja ya vikao vya Bunge mjini Dodoma.

Lissu alisema hayo wakati akisimulia sehemu ya maisha yake binafsi na mambo aliyowahi kukutana nayo maishani katika mahojiano maalumu na Mwananchi yaliyofanyika Jumatano.

Katika simulizi hiyo, Lissu, ambaye kwa sasa ni rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), alizungumzia pia kesi zinazomkabili, maisha ya mahabusu, familia, kazi zake, burudani anazopenda na mahusiano yake na watu wa aina tofauti.

Akizungumzia mkasa uliosababisha anusurike kupata kipigo hicho, Lissu alisema Wasira alikuwa amechukizwa na maneno yake makali bungeni.

“Nilikuwa nimemuudhi kwa kumtolea maneno makali wakati nikichangia,” alisema Lissu akijaribu kukumbuka alichosema.

Pamoja na kutokumbuka alichokisema, wakati huo Lissu alimponda Wasira kuwa alijiunga upinzani kwa kuwa alidhani kuna fedha na alipogundua hakuna ndipo akakimbia kurudi CCM.

“Alichukia sana. Sasa nimetoka pale naenda chooni, nikamkuta akiwa na wabunge wengine wa CCM. Aliponiona akaanza kunifuata akiniambia kuwa atanipiga,” alikumbuka Lissu.

“Akichukia anakuwa mkubwa kweli, na mimi mdogo. Anakuwa tofauti na niliona anaelekeza kwenye kona ili anipate vizuri. Nikiangalia kama wale wabunge wengine wa CCM wataingilia kuamulia, naona hakuna anayetaka kumzuia.

“Nilikuwa natamani mtu aje aingilie, nichomoke, lakini hawakujishughulisha nasi. Akarusha ngumi ya kwanza, nikakwepa. Akanisogelea tena, akarusha ngumi nyingine ikanikosa. Hapo sasa nikawa napiga hesabu. Nikasema akisogea tena, nampiga teke, na akiinama tu kuugulia, mimi nachomoka.”

Hata hivyo, Lissu alisema, Wasira hakuendelea na badala yake akageuka na kuanza kuondoka.

“Hapo ilikuwa pona yangu. Yule anatisha akichukia,” alisema.

Hata hivyo, Wasira amedai Lissu hasemi ukweli.

Lissu analichukulia tukio hilo kuwa la kawaida katika maisha yake ya mapambano ya kutetea mazingira, haki za wanyonge na kupigania demokrasia na utawala bora.

Akijibu swali kuhusu hali ya usalama wake katika maisha anayoendesha ya mapambano, Lissu alisema hajawahi kutishiwa maisha yake kwenye siasa na anakumbuka ni mara moja tu alitishiwa maisha wakati akipigania mazingira.

“Kuna watu wana hasira na mimi kwelikweli, lakini hawajawahi kunitishia,” alisema.

“Nakumbuka zamani kabla sijawa mbaya namna hii, twenty years ago, wakati nikiongoza Chama cha Wanasheria Watetezi wa Mazingira (LEAT) niliwahi kupata vitisho,” alisema Lissu.

Alisema wakati huo Serikali ya Awamu ya Tatu ilimpa raia wa Ireland, Reginald Nolan eneo kwenye delta ya Rufiji ili aendeshe mradi wa kuvuna kamba.

Alisema Serikali ilimpa hekta 20,000 ili atengeneze mabwawa ya kufuga kamba kwenye delta ya Rufiji, maeneo ambayo yana vijiji vinane, shughuli za kilimo na makazi na msitu ya mikoko.

“Niliongoza kampeni ya kimataifa kwa kila njia, ikiwamo mitandao ya kimataifa ya wanaharakati kuupinga mradi huo. Hatimaye, Benki ya Vitega Uchumi ya Ulaya (European Investment Bank) iliyokuwa itoe mkopo kwa Nolan ambao ungedhaminiwa na Serikali ya Tanzania, wakasema hawatatoa mkopo na kwa hiyo, mradi mzima ukasambaratika,” alisema.

“Wakati huo ndipo tukaletewa barua ya vitisho iliyopitishwa chini ya mlango. Asubuhi ndipo tukaikuta. Lakini zaidi ya hapo sijawahi kupata vitisho.

“Kwanza watanitishia nini? Wataniambia nyamaza tutakuua?”

Hata hivyo alisema anajua hayuko salama kutokana na aina ya siasa anazoendesha.

“Huwezi ukawa unaendesha siasa za aina hii halafu ukawa salama. Lazima utegemee kusumbuliwa. Usipotegemea kusumbuliwa, utapata shock,” alisema.

Lissu alisema hata matukio ya kukamatwakamatwa na askari wa Jeshi la Polisi hayajawahi kumshangaza kwa kuwa amekuwa akiendesha siasa za mapambano.

“Na wala sikosi usingizi. Nilale central (kituo kikuu cha poli) au nilale nyumbani, napata usingizi wangu mzuri kabisa,” alisema Lissu.

“Ili mradi nipate chupa zangu tatu kubwa za maji ya Kilimanjaro. Hizi chupa huwa nazitumia kama mto. Nikizipata tu, naweka kichwani na nalala usingizi mzuri kabisa. Tena mimi huwa nakoroma. Ndio maana nikitoka mahabusu huwa mnaniona nimebeba chupa ya maji ya Kilimanjaro.”

Hata hivyo, Lissu alisema hafurahii maisha ya mahabusu kwa kuwa si sehemu nzuri.

“Kusema sikosi usingizi, hakumaanishi kuwa nafurahia kulala mahabusu, hasa unapokuwa huna kosa,” alisema.

“Huko kuna watu wengi wanakamatwa na kuwekwa mahabusu bila ya makosa. Si kitu kizuri.”

Alisema hadi sasa ameshakaa mahabusu kwa kesi nne, ambazo zote ni za uchochezi. Akizungumzia jinsi anavyoweza kumudu maisha ya kifamilia, uwakili, ubunge, uongozi wa Chadema na urais wa TLS, Lissu alisema hayo yote yanawezekana kama unajipanga.

“I’m a very busy man (ni mtu niliye na kazi nyingi), lakini nimejifunza kitu. Fikiria tunatumia muda kiasi gani kwenye kinywaji. Kwa hiyo there’s plenty of time (kuna muda mwingi),” alisema Lissu.

“Napata muda wa TLS, tuna vikao viwili, muda wa kukaa na mama, wa Chadema, na napata muda wa mahakamani, Napata muda wa kinywaji. Mimi nakunywa Tusker ya baridi.

“Ukipanga muda wako sawasawa, there’s plenty of time.”

Lakini alisema kutokana na harakati ambazo zimekuwa zinamkabili, mwaka jana hakupata muda wa kutosha wa kuwa karibu na wapigakura wake wa Jimbo la Singida Mashariki.

“Najua hilo lina gharama zake, lakini ni lazima nifanye kazi zote,” alisema.

Lissu alisema kati ya mambo hayo, hupata muda wa kutosha wa kusoma kwa kuwa hicho ndicho kitu anachokipenda sana maishani mwake.

“Nikisafiri, iwe kwa ndege au kwa gari, ni lazima niwe na vitabu, magazeti. Hata nikiwa gerezani huwa naenda na magazeti,” alisema Lissu.

“Kwa kweli, ikitokea kwamba ninahukumiwa kufungwa, kitu ambacho kitanisumbua sana ni kukosa freedom ya kusoma.”

Lissu amekuwa akihusika katika kesi lukuki, kuanzia zile za kawaida za ofisi yake, za kisiasa zinazohusu wanachama wa Chadema, za wananchi na zinazomkabili, lakini anasema mashauri hayo hayajamfanya awe tajiri.

“Mimi si tajiri, ni mtu wa kawaida. Kazi yangu kubwa ni kutoa msaada wa kisheria,” alisema.

“Nimeoa Tarime, mke wangu ni mwanasheria na anatoka Tarime. Huko mimi ni maarufu sana, lakini si kwa sababu ya mke wangu.

“Huko nilitoa watu 466 gerezani ambao walikuwa wamefungwa kutokana na kupinga kunyang’anywa ardhi.”

Alisema hiyo ilikuwa wakati wawekezaji walipokuwa wakipewa ardhi kwa ajili ya kuchimba madini.

Alisema wateja wake wengine wakubwa kwa sasa ni vijana wanaoshtakiwa kwa makosa ya mtandaoni.

“Sheria mbili za makosa ya mtandaoni zimesababisha watu wengi kukamatwa. Wote wamekuwa wateja wangu,” alisema.

“Usipowatetea hawa wadogo wasio na kitu na wasioweza kusema, siku mkianza kushughulikiwa hakuna atakayewatetea.”

Alisema shughuli hizo huzifanya kwa kutoa msaada na anamudu kufanya hivyo kwa kuwa ni mbunge.

“Mshahara wa ubunge unaniwezesha kutetea Watanzania mahakamani. Fedha kidogo ninayopata ndiyo ninayoitumia kusafiri na gharama nyingine. Si tajiri, lakini naishi confortably,” alisema.

Alisema tofauti na mawakili wengine, kazi yake haina gharama kubwa za uendeshaji kwa kuwa ameziepuka.

“Kwanza ofisi yangu iko nyumbani. Pale ndipo nafanya kila kitu, kwa hiyo hakuna cha kumlipa msichana wa usafi,” alisema mbunge huyo wa Singida Mashariki.

Kuhusu mjadala uliotuama mitandaoni ikimtaja Nape Nnauye kuwa shujaa baada ya kupinga uvamizi wa kituo cha televisheni cha Clouds Media uliofanywa na kiongozi wa Serikali aliyeambatana na askari wenye silaha za moto, Lissu alisema mbunge huyo wa Mtama si shujaa na kumfananisha na waziri wa zamani wa mambo ya ndani wa Ghana, Tawia Adamafyo.

“Huyu mtu amezima Bunge na kulivuruga kwelikweli. Amefungia magazeti. Akiwa waziri amepitisha sheria ya mbovu ya Huduma ya Vyombo vya Habari, sioni ushujaa wowote bali amevuna matunda ya kazi yake na siasa za ndani ya CCM,”alifafanua

Tawia aliwasilisha muswada wa kuwaweka ndani watu enzi za Kwame Nkrumah, sheria ambayo ilipigiwa kelele na wabunge.

“Huyo Tawio hakujua sheria anayotunga inatengeneza rat trap (mtego). Kilichotokea ni yeye kuwa wa kwanza kuwekwa kizuizini kwa kutumia sheria hiyo maofisa usalama kutegesha bomu karibu na eneo alilokuwa akihutbia Rais Nkurumah na hivyo waziri huyo kuonekana alihusika.

“Hawa viongozi wanatunga sheria wanazodhani zitawabana na kuwashughulikia wapinzani, yakiwakuta wao wanapiga kelele. Kwahiyo mimi sioni ushujaa wowote wa Nape,”alieleza Lissu ambaye pia ni mwanasheria mkuu wa Chadema.

Nape alivuliwa uwaziri wa habari Machi 23 baada ya kuachwa kwenye mabadiliko madogo ya Baraza la Mawaziri.

Maalim Seif azidi kumrushia Makombora Lipumba...Safari hii kaja na hili la kummaliza kabisa Lipumba.


VITA vya maneno vimezidi kushika kasi ndani ya Chama cha Wananchi (CUF) na sasa Katibu Mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Sharif Hamad, ameibuka na kumtaka aliyekuwa mwenyekiti wake, Profesa Ibrahim Lipumba, amwache kwa kuwa hana uwezo wa kumfukuza kazi.

Kadhalika, amesema kama kweli Profesa Lipumba anadhani yeye ni mwenyekiti halali, afike makao makuu ya CUF kisiwani Unguja ili kufanya kazi badala ya kukubali aendelee kutumika.

Hivi karibuni Profesa Lipumba alitangaza kumfukuza kazi, Maalim Seif na kumteua Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Tanzania bara, Magdalena Sakaya, kuwa kaimu Katibu Mkuu.

Akizungumza na wananchi na wanachama wa chama hicho katika kisiwa kidogo cha Tumbatu Mvuvini, Maalim Seif alisema anamshangaa Profesa Lipumba kwa madai kwamba yeye ameshindwa kazi kwa kuwa haendi kazini katika ofisi za chama zilikozo Buguruni, Dar es Salaam.

"Eti nimeshindwa kazi akidai kuwa siendi ofisi kuu ya CUF Buguruni. Mbona yeye haji makao makuu ya CUF Mtendeni. Lipumba hana mamlaka ya kuniondoa nafasi yangu ya ukatibu mkuu,” alisema.

Alisema tangu Agosti, 2015, Lipumba hajawahi kukanyaga makao makuu ya CUF Mtendeni na kwamba hata kama angekuwa Mwenyekiti halali wa chama, alipaswa kumwita na kumhoji kwa nini haendi ofisi kuu za chama Buguruni kuliko kuchukua madaraka ya kutangaza kuwa amemtimua.

Maalim Seif pia alikemea siasa za chuki na uhasama zilizotawala kisiwani humo kati ya CCM na CUF na kusema zimesababisha mapigano na hujuma ikiwamo kuchomeana nyumba kutokana na itikadi za vyama.

Naye Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar, Nassor Ahmed Mazrui, alisema Profesa Lipumba ametumika na amefanya kazi kubwa ya kukihujumu chama huku akiungwa mkono na baadhi ya wanachama.

Mazrui pia alimwomba Rais John Magufuli kumtimua Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi, kwa madai kuwa ni miongoni mwa watendaji wabovu wa serikali.

Alisema utendaji mbovu wa Jaji Mutungi umesababisha mtafaruku mkubwa na mgogoro unaoendelea ndani ya CUF.

“Rais Magufuli anatumbua watendaji ambao si waadilifu, lakini Msajili amemwacha kwani anapaswa kutumbuliwa kwa sababu ameivuruga nchi,” alisema.

Alisema Msajili huyo amempa uhalali Profesa Ibrahim Lipumba kuwa mwenyekiti wa CUF, wakati alijiuzulu kabla ya uchaguzi mkuu na sasa amekuwa akikihujumu chama.

Noma Sana..Pamoja na Wakenya Kwenda Mahakamani..Madaktari 470 wa Kitanzania Wajitokeza Kuchangamkia Fursa!


Wakati Mahakama nchini Kenya imezuia kwa muda madaktari kutoka nje kwenda nchini humo kupiga kazi, zaidi 470 wameomba kazi hizo kupitia Wizara ya Afya hapa nchini.

Serikali ya Tanzania imesema mchakato wa kupokea maombi hayo pia utaendelea kwa kuwa haijapokea maelekezo yoyote nchini Kenya.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amesema bado wanasubiri taarifa rasmi kutoka kwa Serikali ya nchi hiyo.

“Tunasubiri taarifa rasmi kutoka Serikali ya Kenya kwa kuwa wao ndiyo walioleta maombi kwetu. Kama kuna mabadiliko yoyote, naamini watatufahamisha rasmi,” amesema.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dk Mpoki Ulisubisya madaktari 470 wametuma maombi kati ya nafasi 500 zilizotangazwa za kwenda kufanya kazi nchini humo.

Msemaji wa wizara hiyo, Nsanchiris Mwamaja amesema: “Tumepokea maombi mengi ya kutosha, lakini ikitokea mtu akatuma tunayapokea, hivi karibuni jopo litakaa na kuanza kupitia maombi hayo kabla ya usaili na baadaye kupanga mipango ya namna gani watafika vituo vyao vya kazi.”


Watu 250 wahofiwa kufa kwenye maporomoko ya ardhi

Mamlaka ya jeshi la Colombia inasema idadi ya waliofariki katika maporomoko ya ardhi nchini humo imefikia watu 250 huku waliojeruhiwa wakiwa 400.
Hata hivyo idadi hiyo huenda ikaongezeka kwani bado kuna zaidi ya watu 200 ambao hawajapatikana .
Vikosi vya wafanyikazi wanaoendesha shughuli za uokoaji wanasema nyingi ya barabara za kulipotekea maporomoko hayo huko eneo la mji wa kusini mwa taifa hilo, Mocoa hazipitiki kutokana na mkasa huo.

Maporomo hayo yametokea baada ya mvua kali kunyesha kwa saa nyingi.
Viongozi wa mataifa jirani wa Mexico na Argentina walikuwa wa kwanza kutoa ujumbe wa pole na kuahidi kwenda kuisaidia Colombia.

Rais Juan Manuel Santosa alitangaza hali ya tahadhari eneo hilo na kusafiri kuangalia shughuli za uokoaji.

Picha zilizochapishwa kwenye mitandao na jeshi zilionyesha baadhi ya majeruhi wakiokolewa kwa kutumia ndege.
Maporomo koya ardhi yamekumba eneo hilo mara kadha miezi ya hivi karibuni.

Mwezi Novemba, watu 9 waliuawa kwenye mji wa El Tambo, karibu kilomita 140 kutoka Mocoa kufuatia maporomoko ya ardhi yaliyosababiswa na mvua kubwa.

CCM na Ukawa Waungana Bungeni Kumsulubu Rais Magufuli..Habari katika Magazeti ya Leo 2/4/2017.





 

Gallery

Popular Posts

About Us