Harufu ya maiti saba Mto Ruvu yafanyiwa kazi | KINGAZI BLOG

HABARI KARIBU YAKO ZAIDI.

Breaking News
Loading...

Sunday 18 December 2016

Harufu ya maiti saba Mto Ruvu yafanyiwa kazi

Dar es Salaam. Siku moja baada ya gazeti hili kuripoti taarifa za kuwapo harufu mbaya na majimaji yanayotoka ilipozikwa miili ya watu saba waliofungwa kwenye viroba, Bibi Afya wa Wilaya ya Bagamoyo, Joyce Nganzo ametembelea eneo hilo kuona hali halisi.

Desemba 8, mwaka huu maiti saba ziliokotwa katika Mto Ruvu na muda mfupi baadaye zilizikwa kando ya mto huo huku Serikali ikiahidi kuendelea na uchunguzi.

Akizungumza na Mwananchi kwa simu jana, Nganzo alisema atakabidhi taarifa ya alichokiona kwa mkurugenzi wa halmashauri ya Bagamoyo kwa ajili ya kuifanyia kazi.

“Nilikwenda, taarifa nitampa Mkurugenzi, yeye ndiyo atakuwa na maamuzi zaidi,” alisema Nganzo.

Katibu wa Kitongoji cha Mtoni, kata ya Makurunge, Mukhtari Shebule alisema,

“Tunashukuru mmeliweka wazi suala hili, bibi afya alikuja kuangalia hali halisi, tunasubiri hatua zitakazochukuliwa kunusuru afya zetu,” alisema Shebule.

Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Hemed Mwanga alisema hana cha kuzungumza na baada ya kukamilika uchunguzi watatoa taarifa.

Kuhusu hali wasiwasi wa usalama kwa wanaotumia maji ya mto huo alisema, “Kuhusu suala hilo sikuwa nalifahamu nitafuatilia nijue unazungumzia nini.”

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Masauni alisema kwa sasa uchunguzi wa suala hilo unaendelea na taarifa ya awali imeshatolewa na bosi wake, Mwigulu Nchemba.

“Muwe na subira kwa sasa , hadi hapo uchunguzi utakapokamilika mtapewa taarifa,” alisema.

Waziri Nchemba hakupatikana kuzungumzia hatua zilizofikiwa hadi sasa na simu yake iliita bila kupokea.

google+

linkedin

About Author
  • BLOG NAMBA MMOJA KWA MATANGAZO YA AJIRA NA NAFASI ZA KAZI TANZANIA. Soma zaidi

    0 comments:

    POST A COMMENT

     

    Gallery

    Popular Posts

    About Us